Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango ya Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ imefanya ziara maalum katika Halmashauri ya Jiji la Mwanza kwa lengo la kujifunza mbinu za kisasa na bora za ukusanyaji wa mapato ya ndani. Ziara hiyo ililenga hasa kuangazia namna ya uendeshaji wa stendi za mabasi kama chanzo muhimu cha mapato kwa halmashauri.
Katika ziara hiyo, wajumbe wa kamati hiyo wakiongozana na wataalamu wa Halmashauri, pamoja na wakuu wa idara na vitengo mbalimbali, walipata fursa ya kutembelea Stendi ya Mabasi ya Nyegezi. Walijifunza kwa vitendo jinsi mfumo wa ukusanyaji mapato unavyofanya kazi kwa ufanisi, pamoja na kupokea maelezo ya kina kutoka kwa Meneja wa stendi hiyo kuhusu taratibu, mifumo ya kidigitali inayotumika, na hatua zinazochukuliwa kuhakikisha uwazi na ufanisi katika ukusanyaji huo.
Meneja wa stendi ya Nyegezi alieleza jinsi mfumo wa uendeshaji wa stendi hiyo unavyosaidia kuongeza mapato ya halmashauri kwa njia ya uwazi, kuzuia mianya ya upotevu wa mapato, na kurahisisha upatikanaji wa takwimu kwa ajili ya mipango ya maendeleo. Wageni kutoka Hanang’ walionesha kuvutiwa na mifumo hiyo na kueleza kuwa wana nia ya kuiga baadhi ya mbinu hizo pindi watakaporejea kwao.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Hanang’, Bi Teresia Irafay, ziara hiyo ni sehemu ya mkakati wa kujengea uwezo halmashauri hiyo katika kusimamia vyanzo vyake vya mapato kwa ufanisi. Ameeleza kuwa uboreshaji wa ukusanyaji wa mapato ni msingi wa utoaji wa huduma bora kwa wananchi, na kwamba halmashauri itaendelea kuwahamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika ulipaji wa kodi na tozo mbalimbali.
Kupitia ziara hii ya mafunzo, Hanang’ inalenga kuimarisha usimamizi wa rasilimali zake kwa kutumia mifumo ya kisasa na kushirikiana na halmashauri nyingine nchini ili kubadilishana uzoefu. Hatua hii inaonesha dhamira ya dhati ya viongozi wa Hanang’ kuboresha utendaji wa halmashauri na kuhakikisha kuwa wananchi wananufaika na huduma stahiki kutokana na mapato yao ya ndani.
Hanang' District Council Headquater located at the Northern part of Katesh town in Ganana Ward
Postal Address: P.O Box 02 Katesh-Hanang'
Telephone: 027-2530022 / 42
Mobile: +255 762 362 950
Email: ded@hanangdc.go.tz
Copyright ©2016 GWF . All rights reserved.