Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang Teresia Irafay, ameiaga rasmi timu yake ya wanafunzi 120 watakaoiwakilisha wilaya ya Hanang kwenye mashindano ya michezo ya shule za msingi (UMITASHUMTA) ngazi ya mkoa, yatakayofanyika kimkoa katika Wilaya ya Babati.
Katika hafla fupi lakini yenye hamasa, iliyofanyika Mei 28, 2025, katika shule ya msingi Katesh A, Irafay amewaaga vijana hao waliopatikana kupitia mchujo wa makini kwenye shule za msingi wilayani hapa.
“Ninajivunia kuona kizazi cha leo kinapata nafasi ya kuonyesha vipaji vyake katika medani ya michezo. Nidhamu yenu itawavusha mbali zaidi ya ushindi wa Babati,” alisema Irafay huku akiahidi kuwa halmashauri itaendelea kuwaunga mkono washiriki hao kwa hali na mali.
Irafay pia amewapongeza walimu kwa kazi kubwa ya kuandaa timu hiyo, akieleza kuwa maandalizi madhubuti ni msingi wa mafanikio akisisitiza kuwa michezo ni zaidi ya ushindani na ni daraja la kukuza nidhamu, umoja, na afya ya mwili na akili kwa watoto.
Kwa upande wake, Afisa Elimu Msingi wa Wilaya ya Hanang, Geofrey Abayo, ametoa shukrani kwa Mkurugenzi kwa kuhakikisha vifaa vya michezo vinapatikana kwa wakati. “Motisha hii imewajengea wanafunzi hali ya kujiamini. Tuna imani tutarejea Hanang tukiwa tumebeba vikombe,” alisema Abayo kwa matumaini makubwa.
Mashindano ya UMITASHUMTA kwa wilaya ya Hanang, mwaka huu si tu ni nafasi ya kushindana, bali ni mwendelezo wa uwekezaji wa wilaya katika kukuza michezo kuanzia ngazi ya shuleni.
Hanang' District Council Headquater located at the Northern part of Katesh town in Ganana Ward
Postal Address: P.O Box 02 Katesh-Hanang'
Telephone: 027-2530022 / 42
Mobile: +255 762 362 950
Email: ded@hanangdc.go.tz
Copyright ©2016 GWF . All rights reserved.