Mkrugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang, Teresia Irafay, leo ameongoza kikao cha tathmini ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo tofauti ya wilaya hiyo.
Kikao hicho kililenga kutathmini hatua zilizofikiwa, changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya kuhakikisha miradi yote inakamilika kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha.
Akizungumza katika kikao hicho, Irafay amewatia moyo wasimamizi wa miradi kwa juhudi wanazozifanya kuhakikisha kuwa miradi inatekelezwa kwa wakati na kwa kuzingatia viwango vya ubora.
“Nawapongeza sana kwa kazi kubwa mnayofanya. Hata hivyo, nawahimiza kuendelea kuzingatia ubora, kuweka nyaraka zote muhimu na kuhakikisha miradi inatunzwa ipasavyo mara tu inapokamilika,” alisema Mkurugenzi Irafay.
Aidha amesema wasimamizi ambao taarifa zinaonesha ujenzi uko chini ya 50% wasipomaliza miradi hiyo kabla ya mwisho wa mwezi Juni 2025 atawawajibisha ipasavyo.
Kikao hicho, ambacho ni cha pili kufanyika ndani ya kipindi cha miezi mitatu, ni sehemu ya mkakati wa halmashauri kuhakikisha kuwa hakuna mradi unaochelewa au kuachwa njiani, hususan ikizingatiwa kuwa mwaka wa fedha unakaribia kuisha.
Baadhi ya watendaji wa ngazi ya vijiji na kata wamemshukuru Mkurugenzi kwa kuwa karibu nao na kwa kuwapatia moyo kupitia vikao vya aina hiyo.
“Kwa kweli kikao hiki kimetupa ari mpya. Tunajisikia kuthaminiwa na tunajua kazi tunayofanya inaonekana. Tunamshukuru Mkurugenzi kwa kutusikiliza na kututia moyo,” alisema Mwalimu Mwangesi wa Bassotu.
Hanang' District Council Headquater located at the Northern part of Katesh town in Ganana Ward
Postal Address: P.O Box 02 Katesh-Hanang'
Telephone: 027-2530022 / 42
Mobile: +255 762 362 950
Email: ded@hanangdc.go.tz
Copyright ©2016 GWF . All rights reserved.