Stendi mpya ya mabasi ya Katesh Bus Terminal iliyopo mji wa Katesh wilaya ya Hanang, inatarajiwa kuanza kutumika rasmi kesho, Mei 27, 2025, kwa shughuli zote za usafirishaji wa abiria.
Akizungumza wakati wa kikao na wadau mbalimbali wa usafirishaji, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang, Teresia Irafay, alieleza kuwa maandalizi yote muhimu yamekamilika ikiwa ni pamoja na kutangaza rasmi meneja wa stendi hiyo mpya.
Kwa mujibu wa utaratibu mpya uliowekwa na halmashauri, mabasi yote makubwa, madogo na magari mengine ya abiria yatatakiwa kuondoka na kuwasili kupitia stendi hiyo pekee.
Irafay amesisitiza kuwa haitaruhusiwa tena magari ya abiria kupakia au kushusha abiria katika maeneo yasiyo rasmi, hatua inayolenga kudhibiti uchafuzi wa mazingira na msongamano wa magari katika mji wa Katesh.
Aidha, ametoa wito kwa wamiliki wa magari, madereva, mawakala wa mabasi na wafanyabiashara kuzingatia sheria, taratibu na miongozo ya matumizi ya stendi hiyo na kusisitiza umuhimu wa kudumisha usafi katika eneo hilo ili kulinda afya za watumiaji na kulifanya jiji kuwa na mandhari ya kuvutia.
Hatua hii inalenga kuboresha huduma za usafiri, kuongeza usalama wa abiria na kuchangia katika mpango wa kupendezesha mji wa Katesh kwa kuondoa maeneo holela ya upakiaji na ushushaji abiria.
Hanang' District Council Headquater located at the Northern part of Katesh town in Ganana Ward
Postal Address: P.O Box 02 Katesh-Hanang'
Telephone: 027-2530022 / 42
Mobile: +255 762 362 950
Email: ded@hanangdc.go.tz
Copyright ©2016 GWF . All rights reserved.