Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang, Teresia Irafay, ametoa wito kwa wananchi kuendeleza utamaduni wa kufanya usafi bila kushurutishwa, hasa katika maeneo ya biashara na mijini, akisisitiza kuwa mazingira safi huvutia wateja, hupendezesha mji na kusaidia kudhibiti magonjwa ya mlipuko.
Irafay ametoa rai hiyo aliposhiriki mkutano wa Baraza la Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katesh, uliojadili masuala mbalimbali ikiwemo usafi wa mazingira, kudhibiti uhalifu na kuhamasisha maendeleo ya mji kwa ujumla.
Aidha, ametoa onyo kwa wamiliki wa maduka ya bidhaa ngumu wanaokiuka masharti ya leseni kwa kuuza mboga mboga na matunda, akisema hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao akisisitiza kuwa leseni za biashara hizo zitafungiwa kwa mujibu wa taratibu, kwani hali hiyo inachangia uchafuzi wa mazingira na kuvuruga mpangilio wa biashara katika mji.
Katika mkutano huo, Afisa Mtendaji wa Mamlaka ya Mji Mdogo Katesh, Daudi Manda, kwa kushirikiana na wajumbe wa baraza, walikubaliana kuchukua hatua madhubuti dhidi ya mifugo inayozurura au kuchungwa katikati ya mji.
Azimio hilo linakwenda sambamba na marufuku ya wazi dhidi ya ufugaji holela katika maeneo ya mamlaka ya mji huo ambapo Manda ameeleza kuwa hatua hizo zinalenga kulinda heshima ya mji na kuhakikisha mazingira yanakuwa safi, salama na yenye hadhi inayolingana na Mamlaka ya Mji Mdogo.
Hanang' District Council Headquater located at the Northern part of Katesh town in Ganana Ward
Postal Address: P.O Box 02 Katesh-Hanang'
Telephone: 027-2530022 / 42
Mobile: +255 762 362 950
Email: ded@hanangdc.go.tz
Copyright ©2016 GWF . All rights reserved.