Katika hatua inayotajwa kuwa ya kihistoria kwa baadhi ya vijiji vya Wilaya ya Hanang’, Serikali imekabidhi rasmi hati za umiliki wa ardhi kwa wananchi wa kata za Ishponga na Masakta, hatua iliyowasha mwanga mpya wa matumaini miongoni mwa wakazi wa maeneo hayo, hususan katika nyanja za usalama wa miliki, uwezeshaji kiuchumi, na kupunguza migogoro ya ardhi iliyodumu kwa miaka mingi.
Zoezi hilo limefanyika Aprili 29, 2025 kwa uongozi wa Katibu Tawala wa Wilaya ya Hanang’, Mwalimu Athuman Likeyekeye, aliyesisitiza umuhimu wa nyaraka hizo kama chombo halali cha kumtambua mmiliki wa ardhi na daraja la maendeleo kwa familia nyingi vijijini.
"Hati hizi ni zaidi ya makaratasi, ni hazina. Zinalinda haki zenu, zinatoa fursa kwa taasisi za kifedha kuwakopesha, na ni urithi halali kwa vizazi vyenu," alisema Mwalimu Likeyekeye akiwaasa wananchi kuzitunza kwa uangalifu na kutozichezea.
Kulingana na taarifa ya Kaimu Mkuu wa Idara ya Ardhi wilayani humo, Erick Erasmus Mbeya, mashamba zaidi ya yamepimwa tayari, ikiwa ni asilimia 96 ya lengo katika kata hizo mbili. Ameeleza kuwa mafanikio hayo yametokana na usimamizi thabiti wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’, Teresia Irafay, ambaye amekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kila mwananchi anapata haki yake ya msingi ya kumiliki ardhi kwa mujibu wa sheria.
Mbeya ameongeza kuwa juhudi hizi ni sehemu ya mpango mpana wa kitaifa wa kuhakikisha usalama wa miliki na uendelezaji wa ardhi kwa njia endelevu, huku Halmashauri ya Hanang’ ikitajwa kuwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa kasi ya utekelezaji.
Kwa upande wao, wananchi waliokabidhiwa hati hizo wameelezea furaha yao kwa kauli mbalimbali za shukrani, wakitaja manufaa wanayotarajia kuyapata, ikiwemo uwezo wa kuchukua mikopo kwa ajili ya shughuli za kilimo, biashara ndogo ndogo, pamoja na uhakika wa kupangilia maendeleo ya familia zao bila hofu ya kupokonywa ardhi kiholela.
"Kwa sasa naweza kujenga bila woga, najua hii ni yangu kisheria. Pia nitamwachia mwanangu kitu chenye thamani na heshima," alisema mmoja wa wakazi wa Masakta.
Zoezi hili linajiri wakati ambapo nchi nzima inasisitiza mpango bora wa ardhi kama msingi wa maendeleo, huku migogoro ya ardhi ikiwa ni changamoto sugu inayochochea migogoro ya kijamii na kudhoofisha ustawi wa wananchi wengi wa vijijini.
Hatua ya Halmashauri ya Hanang’ imepokelewa kama mfano bora wa utekelezaji wa sera kwa vitendo, na tayari imekuwa ikitazamwa na maeneo mengine kama mwanga wa mabadiliko chanya ya mfumo wa usimamizi wa ardhi vijijini.
Hanang' District Council Headquater located at the Northern part of Katesh town in Ganana Ward
Postal Address: P.O Box 02 Katesh-Hanang'
Telephone: 027-2530022 / 42
Mobile: +255 762 362 950
Email: ded@hanangdc.go.tz
Copyright ©2016 GWF . All rights reserved.