Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ inaendelea kutekeleza kwa vitendo dhamira yake ya kuboresha mazingira ya utoaji wa elimu nchini, kwa kuwekeza katika miundombinu ya shule katika maeneo yenye uhitaji mkubwa.
Kwa sasa, jitihada hizo zimejikita katika ujenzi wa Shule Mpya ya Msingi Hararak, iliyopo katika Kata ya Gendabi, Wilaya ya Hanang’. Mradi huu unatekelezwa kwa gharama ya Shilingi milioni 348.5 kwa ufadhili wa Serikali Kuu, na unahusisha ujenzi wa vyumba saba vya madarasa, jengo la utawala, madarasa mawili ya shule ya awali, na vyoo vya kisasa. Ujenzi unatarajiwa kukamilika ifikapo tarehe 30 Mei, 2025.
Kwa muda mrefu, watoto kutoka kitongoji cha Hararak walilazimika kutembea umbali mrefu kufuata elimu katika Shule ya Msingi Dumanang, hali iliyosababisha changamoto katika mahudhurio, utoro na uchovu kwa watoto hasa wa darasa la awali. Aidha, ongezeko la wanafunzi katika shule mama ya Dumanang lilizidi uwezo wake wa kawaida.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’, Teresia Irafay, amesema kuwa ujenzi wa shule hii ni sehemu ya mpango mpana wa Serikali wa urejeshaji wa huduma kwa wananchi, hasa katika maeneo yaliyokumbwa na janga la maporomoko ya tope yaliyotokea Desemba 3, 2023.
“Serikali imejizatiti kuhakikisha kuwa kila mtoto anapata elimu katika mazingira salama, rafiki na yanayochochea maendeleo ya kitaaluma. Tunaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi hii ili ifikie malengo yaliyokusudiwa kwa wakati,” amesema Irafay.
Wananchi wa Hararak wameipokea kwa furaha hatua hii ya serikali. Dorika Nantanga, mkazi wa eneo hilo, amesema kuwa ujio wa shule hiyo umerejesha matumaini kwa wazazi na watoto. “Tulikuwa tunahangaika kuwapeleka watoto mbali, lakini sasa huduma iko karibu. Hili ni jambo la kumshukuru Mungu na Serikali,” alisema.
Ujenzi wa shule hii mpya pia unatarajiwa kuongeza uandikishaji wa watoto wa awali na elimu ya msingi, kupunguza utoro, na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa ujumla.
Mradi huu ni miongoni mwa hatua madhubuti zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuhakikisha azma ya “Elimu kwa Wote” inatekelezwa kwa vitendo na kwa usawa katika maeneo yote ya nchi.
Hanang' District Council Headquater located at the Northern part of Katesh town in Ganana Ward
Postal Address: P.O Box 02 Katesh-Hanang'
Telephone: 027-2530022 / 42
Mobile: +255 762 362 950
Email: ded@hanangdc.go.tz
Copyright ©2016 GWF . All rights reserved.