Katika lengo la kuboresha utoaji wa huduma katika stendi mpya ya mabasi ya Katesh, Halmashauri ya Wilaya ya Hanang imekutana na uongozi wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi Mkoa wa Manyara (MABOA) kujadili changamoto, fursa na mikakati ya usimamizi bora wa kituo hicho cha kisasa.
Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang, Teresia Irafay, amesisitiza dhamira ya halmashauri kuendelea kushirikiana na wadau wa sekta ya usafiri ili kuhakikisha maboresho ya stendi hiyo yanakwenda sambamba na mahitaji halisi ya wananchi.
Ameahidi kufanyia kazi hoja na mapendekezo yaliyowasilishwa na viongozi wa MABOA, ikiwemo kuongeza vituo vya muda kwa ajili ya kupakia na kushusha abiria nje ya stendi, hatua itakayopunguza usumbufu kwa wasafiri na kuboresha mtiririko wa magari ndani ya mji.
Aidha, Irafay ametoa rai kwa wamiliki wa mabasi na wafanyakazi wao kuzingatia sheria na taratibu za usafirishaji, akisisitiza kuwa mabasi yote yanapaswa kuingia stendi rasmi na kuacha tabia ya kupakia au kushusha abiria kiholela, ambayo inaweza kuhatarisha usalama wa abiria na kuvuruga mpangilio wa usafiri.
Kwa upande wao, viongozi wa MABOA wamepongeza jitihada za halmashauri katika kuanzisha stendi hiyo ya kisasa, wakitambua kuwa ni hatua muhimu katika kukuza uchumi wa wilaya na kuboresha mazingira ya kazi kwa watoa huduma wa sekta ya usafiri na kuahidi kuendelea kushirikiana kwa karibu na halmashauri katika kuhakikisha kanuni za uendeshaji wa stendi hiyo zinafuatwa ipasavyo.
Stendi ya Katesh imejengwa kama sehemu ya mkakati mpana wa halmashauri ya Hanang wa kuboresha huduma za uchukuzi, kuimarisha miundombinu na kuongeza mapato ya ndani kupitia usimamizi makini wa sekta ya usafiri.
Hanang' District Council Headquater located at the Northern part of Katesh town in Ganana Ward
Postal Address: P.O Box 02 Katesh-Hanang'
Telephone: 027-2530022 / 42
Mobile: +255 762 362 950
Email: ded@hanangdc.go.tz
Copyright ©2016 GWF . All rights reserved.