Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang, Teresia Irafay, amekutana na wamiliki wa viwanda vya kuchakata alizeti katika wilaya ya Hanang kwa lengo la kujadili njia bora za kudhibiti na kusimamia ushuru unaotokana na zao hilo la biashara.
Katika kikao hicho, Mkurugenzi amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya sekta binafsi na halmashauri katika kuhakikisha mapato yote stahiki yanapatikana, huku akieleza kuwa usimamizi thabiti wa ushuru ni njia mojawapo ya kuongeza kipato cha halmashauri na kuchochea maendeleo ya wananchi.
Wakizungumza katika kikao hicho, wamiliki wa viwanda vya kukamua alizeti wameahidi kushirikiana kwa karibu na halmashauri pamoja na wadau wengine ili kuhakikisha kuwa serikali inakusanya mapato yote yatokanayo na mnyororo mzima wa thamani wa alizeti kuanzia shambani hadi kiwandani.
Wamesema kuwa wanaunga mkono jitihada za halmashauri katika kuweka mifumo madhubuti ya ukusanyaji mapato, na kuahidi kuwa watatoa ushirikiano wa karibu katika kuhakikisha hakuna upotevu wa mapato unaojitokeza katika sekta hiyo.
Zao la alizeti ni miongoni mwa mazao makuu ya biashara yanayolimwa kwa wingi wilayani Hanang, na lina mchango mkubwa katika uchumi wa wananchi pamoja na halmashauri kwa ujumla.
Hanang' District Council Headquater located at the Northern part of Katesh town in Ganana Ward
Postal Address: P.O Box 02 Katesh-Hanang'
Telephone: 027-2530022 / 42
Mobile: +255 762 362 950
Email: ded@hanangdc.go.tz
Copyright ©2016 GWF . All rights reserved.